Member of EVRS

Friday 18 February 2011

Rwanda: Kuanza Kufundisha Masomo kwa Kinyarwanda Kwenye Shule za Msingi

Hivi karibuni Nchi ya Rwanda imeamua kuanza kufundisha masomo ya shule za Msingi kwa Kinyarwanda, na pindi watotot watakapoingia shule za sekondari ndio wataanza kujifunza masomo yote kwa kiingereza.

Hatua hii imekuja muda si mrefu sana tangu Serikali ya Rwanda kubadili ghafla mfumo wa masomo na lugha rasmi kitaifa kutoka kwenye lugha ya kifaransa na kuingia katika lugha ya kiingereza.  
 
Nia na madhumuni ya kuanza kufundisha kinyarwanda shule za msingi, ni pamoja na kukuza lugha asili na pia kuwapa nafasi watoto kujifunza kikamilifu sarufi na mambo mengine kadhaa ya kinyarwanda. 
  
Kwa sisi wageni, na baadhi ya wanyarwanda waliozaliwa na kukulia nje ya Rwanda, huwa tunapata changamoto kusoma maandishi ya lugha hii, kwani mengine yanavyo andikwa na kutamkwa ni tofauti kabisa. 
  
Nimeshashuhudia baadhi ya wanyarwanda wakisoma matangazo kwa kinyarwanda, na kufikia mahali wasijue neno fulani lina maana gani kutokana na tofauti kati ya maandishi na yanavyotamkwa.  
  
Natoa mfano rahisi kabisa, jina Kacyiru hutamkwa kama "kaachiru", na neno lingine kama Kimicanga hutamkwa kama "Chimichanga", na kali kidogo ni Kimironko ambalo hutamkwa kama "Chimirong'o", nyingine yenye ka-ugumu kiasi ni Kicukiro wao wanatamka "Chichuchiro".
Hii ni mifano tu, bado kuna nyingine ngumu zaidi. 
  
Kuna baadhi ya watu wameanza kulalamika na suala la kubadili kwa haraka lugha za mawasiliano na kufundisha, lakini kwangu mfumo huu wa shule naona hauna tofauti sana na ule tulio nao nyumbani Tanzania, kwani nasi shule za msingi tunatumia kiswahili, japo kuna wachache wameanza kuvuruga matunda ya vijana wetu wanaomaliza sekondari kwa kuwapika nusu nusu na kutoka wakiwa wabichi.  
  
Nawatakia mapumziko mema ya mwisho wa wiki!

3 comments:

Simon Kitururu said...

Wanaanza mfumo ambao TANZANIA inaonekana kutaka kuuacha?

Kwa maana nasikia siku hizi wajanja wote watoto wao wanaanza kusoma kwa Kiingereza na Kifaransa tokea shule ya vidudu!

Hivi kuna shule zinafundisha KICHINA Tanzania kwa kuwa inasemekana future iko CHINA?

chib said...

Ha ha haa Simon, kichina!!! Pamoja na kuwa wachina wapo mabilioni, lakini bado kichina chao kimegawanyika mafungu mafungu, halafu tatizo ni kuwa maandishi yao ni kama mkusanyiko wa maboksi boksi, watoto wataona kama ni mzaha tu

Goodman Manyanya Phiri said...

@chib: Kumbe siyo hivyo Mkuu Chib! Lazima Wachina nao watakuwa naKichina rasmi ingawaje wamegawanagawana. Hata katika ka uchumi inasemekana USA "wapi tena kuona ndani"!


Kuhusu maandishi ya Kichina, ndio yatakuwa magumu kujifunza; lakini hata Kiingereza, pamoja na herufi tuliyezowea, NI MOJA YA LUGHA NGUMU SANA ULIMWENGUNI KUMANYA!


@Kitururu: Hao Waswahili "wakubwa" zetu wanaojaribu kuwabadili Wazungu watoto wao wamezagaa kote Barani. Afrika Kusini wamekwishawaondoa kabisa watoto wao maeneo ya Uswahilini kama Soweto na wanakwenda wangalibado wadogo kujifunza Kiingereza na Wazungu. Mwishowe mtoto huyo ("COCONUT" au "nazi" kama wanavyoitwa hapa kwetu) anakuwa kwa nje Mwafrika ndiyo aliyesoma lakini ndani yake (ndani ya nazi kweupe)anao utamaduni wa Ulaya na anawauzia Bara Afrika Wakoloni mambo-leo. Hao viongozi COCONUT ndio waliyosababisha Waafrika kuwashambulia Waafrika wenzao hapa kwetu kwa kuwa Kiongozi COCONUT hathamini Uafrika wake! THEY HAVE BEEN BRAINWASHED.


Wachina bado wanadharaurika sana mbele za hao watoto na wazazi wao COCONUT, kwani kiumbe kiliyekamilika mbele za macho yao "ni Mzungu tu".