Member of EVRS

Monday 6 July 2009

Siku ya Kukumbuka Ukombozi wa Rwanda



Photo above: Mwalimu Julius Kambarage Nyerere

Juzi hapa Rwanda ilikuwa ni siku ya kukumbuka ukombozi wa Rwanda kutoka katika mauaji ya kimbari miaka 15 iliyopita.

Kwa kawaida kila mwaka hutolewa zawadi za kijadi kwa mashujaa wa Rwanda katika matukio mbalimbali. Mwaka huu ilikuwa ni tofauti kidogo, kwani mashujaa waliotoa mchango mkubwa katika kumaliza vita hivyo, nao walipewa nishani za heshima za uruti ambayo hupewa mashujaa waliotukuka wa Rwanda, na Umurinzi, ambayo ni kwa wale wanaoshiriki kikamilifu katika kampeni ya kutokomeza mauaji ya kimbari Rwanda.

Mwaka huu watu watatu wamepata nishani hizo akiwemo Waziri mkuu wa Ethiopia Menan Zenawi, Rais wa Uganda Yoweri Kaguta Museveni na Hayati Baba wa Taifa, Julius Kambarage Nyerere ambaye nishani yake ilichukuliwa na mjane wake Mama Maria Nyerere
Kwangu nilijihisi kupata heshima kubwa pamoja na Taifa langu la Tanzania kwa wananchi wa Rwanda kutambua juhudi za Baba wa Taifa katika kwa kuwa mtu wa mwanzo kukemea mauaji yaliyokuwa yakiendealea Rwanda mwaka 1994 ingawa hakuwa kiongozi wa nchi.

Pia katika wasifu wake ambao ulisomwa kwa Kiswahili umeonyesha ni jinsi gani wanyarwanda wanavyomuenzi katika ukombozi wao. Pia waliwasifia sana watanzania kwa moyo wao mkarimu wakati wote walipokuwa katika hali ya ukimbizi, kiasi kwamba walijisikia kama wapo kwao, maana kulikuw hakuna ubaguzi wa aina yoyote katika elimu, matibabu mpaka na kazi.

Naye Yoweri Musevani katika hotuba yake fupi, mbali ya kueleza historia ya mapambano, na mchango wa Uganda, hakusita kuchukua sehemu ya hotuba yake kuishukuru Tanzania kama nchi pekee katika Afrika iliyotoa mazingira ya kiurafiki (non hostile environment) wakati wa tatizo la mauaji. Pia alielezea historia ndefu ya Tanzania katika kupambana ili kuleta Uhuru katika nchi z Afrika ikiwa ni pamoja na Uganda.

Paul Kagame wa Rwanda, naye alichukua nafasi ya hotuba yake kutoa shukrani zake za dhati kwa Nyerere na watanzania kwa ujumla.
Mpaka juzi asubuhi, sikuwa najua ni jinsi gani wanyarwanda wanavyowathamini na kuwaenzi watanzania katika ukombozi wao dhidi ya mauaji ya kimbari.

2 comments:

Simon Kitururu said...

Mie sikujua kuwa WaTZ wanathaminiwa hivyo huko Rwanda. Nashukuru kwa habari hii MKUU!

Anonymous said...

Nami naungana na Simon, nimefurahi kabisa kusikia habari hii. Nafikiri ni lazima nifike Rwanda