Member of EVRS

Sunday 25 July 2010

Mkutano wa Watanzania waishio Rwanda

Jana tarehe 24 julai 2010, umoja wa Watanzania waishio Rwanda tulikutana kama kalenda yetu ilivyokuwa imepanga, ulikuwa ni mkutano wa kwanza baada ya kuanzisha rasmi umoja huu ambao kwa ufupi unaitwa UTARWA na ulifanyika katika eneo la ubalozi wa Tanzania, Rwanda.

Uongozi mpya wa umoja huu chini ya Mwenyekiti wetu Mama Josephine Marealle-Ulimwengu (Katikati katika picha hii chini) ulipanga mikakati mbalimbali ya kuuendeleza umoja huu katika mpangilio maalumu wenye viambatanisho na ufuatiliaji wa matukio mbalimbali ya umoja, ikiwa ni pamoja na malengo yanayokusudiwa kwa muda maalumu. Katika masuala muhimu yaliyojadiliwa ilikuwa ni pamoja na kuwa na ofisi ya kudumu ikiwa pamoja na samani, tovuti, na pia kuanzisha klabu kwa ajili ya kubadilishana mawazo na pia kuandaa matamasha ya michezo hasa ya kujenga afya.


Watanzania kwa umoja wao, waliweza kuchanga papo hapo pesa ambazo zilitosha kununulia mashine ya kudurufu karatasi.


Uongozi wa UTARWA, pia uliweka wazi kwa majadiliano mti wa mawasiliano waliouandaa, ambao utaweza kuunda mtandao wa Watanzania wote wanaoishi Rwanda. Njia hii itawezesha mawasiliano kuwa ya haraka.

Pichani juu, maelezo kuhusu mti wa mawasiliano yakitolewa kwa wajumbe wote ndani ya ofisi ya ubalozi wa Tanzania, Rwanda.
Shughuli nyingine ambayo uongozi umekuwa ukifanya, ni kuandaa tovuti ambayo itakuwa na taarifa za wanachama wote, ikiwa ni pamoja na familia zao kadri mwanachama atakavyojaza kwenye fomu maalumu ya kuingia uwanachama. Na hii data base itakuwa inaweza kuonwa na viongozi tu, iwapo mwanachama atataka taarifa zake, basi ataweza kuzipata.

Pichani juu, wakati wa utambulisho wa tovuti ya UTARWA, ambayo itakuwa na taarifa nyingi za nyumbani, hapa Rwanda, habari za magazeti na blogu mbalimbali.


Pichani juu, baadhi ya wajumbe wa UTARWA wakisikiliza kwa makini maelezo yanayohusiana na tovuti.
Katika shughuli zilizopangwa baadaye, ni kuchangisha pesa ili kutunisha mfuko wa jumuiya ya akina Mama wa Kitanzania waishio Rwanda, na vitaandaliwa vyakula maalumu vya kitanzania hapo tarehe 3 oktoba 2010.



4 comments:

Fadhy Mtanga said...

Hongereni sana kwa hatua mliyoifikia. Umoja ni silaha muhimu sana katika maendeleo.

Nakutakieni kila la kheri.

Anonymous said...

Natamani nami ningekuwa Rwanda!

John Mwaipopo said...

hongereni. leteni hoja kuwa watanzania waishio nje ya nchi waruhusiwe kupiga kura wakati wa uchaguzi. mnaweza kushindwa kwa mwaka huu lakini inshaalah kwa miaka ijayo. wanywarwanda waishio nje ya nchi yao wanatwanga kura nyumbani, au siyo?

chib said...

@Fadhy and anony... thanks
@ Mwaipopo... utafikiri ulikuwepo kwenye mkutano huu