Member of EVRS

Friday 4 June 2010

Kudhibiti Uhalifu: Tanzania Yapaswa Kujifunza Kutoka Kwa Rwanda

Tukio la hivi karibuni la watu kuchoma moto kituo cha polisi huko Mkoani Kilimanjaro ni la kusikitisha sana, ukipenda waweza kuliita la kuudhi sana.

Sababu kubwa ya uchomaji wa kituo hicho cha polisi kwangu mimi siielewi, kwani taarifa zinajikanganya.

Kituoni humo walikuwepo watuhumiwa waliokuwa wanadaiwa kumteka na kumuua mtoto kwa shughuli za kafara, lakini kimsingi tuhuma hizo hazikuwa sahihi, kwani mtoto alipatikana siku iliyofuata akiwa Moshi, tena mzima na buheri wa afya!

Tukio ambalo ni la aibu, ni kuona kuwa polisi wa Tanzania hawako au hawakuwekwa katika mazingara ya kuwa imara kuweza kudhibiti wahalifu wawapo vituoni mwa polisi, kwani vituo vingi ni majengo tu, na polisi wenyewe mbali ya kuwa ni waoga, lakini pia hawana vifaa vya kujilinda kwa matukio ya uvamizi kama huo.

Lakini pia mfumo wa nchi yetu umelitelekeza jeshi la polisi wakati matukio ya uhalifu ni mengi.

Kwa mtizamo wangu ningeishauri serikali yetu kuweza kuiga mfano wa Rwanda, ambao hulitumia jeshi la wananchi wa Rwanda kushiriki katika ulinzi wa mali na usalama wa watu sehemu mbalimbali hasa nyakati za usiku, ambapo hufanya doria wakiwa wana silaha za moto za kujilinda dhidi ya waalifu na waleta vurugu.

Utakuta wanazunguka mitaani usiku, tena kwa mpango maalumu ambapo hata ukiwashambulia, huwezi kuwapata wote kwani hawaendi kiholela kama kuku. Na wanapita sehemu zote zenye mikusanyiko ya watu kama sehemu za starehe, supermarkets, makazi ya watu, hospitali kubwa na maeneo ya masoko.

Kwa Tanzania, mbali ya kuwa polisi hawatoshelezi maeneo yote, lakini jeshi hilo limeachiwa pekee jukumu la kuangalia usalama wa ndani ya nchi, ikiwa ni pamoja na kudhibiti watekaji wa magari wakati wa usiku kwenye mapori, na wakati huo huo jeshi la wananchi wapo majumbani wamelala, na hivyo kuwapa fursa kwa baadhi yao kushiriki katika uhalifu, au kupiga wananchi bila sababu za msingi.

Tunapaswa kuondoa dhana ya kuwa wanajeshi kazi yao ni kwenye vita tu, bali katika kipindi hiki cha "utulivu kwa jina" watumike katika kudhibiti matukio ya uhalifu hasa maeneo ya mipakani sehemu za Kigoma na Kagera ambako wezi hutoka nchi za jirani wakiwa na silaha nyingine za kivita na kuendesha uhalifu kwetu, na pia mijini maeneo ambayo yamekithiri kwa visa vya uporaji na kushambulia wananchi.
Kwa mantiki hii kutasaidia kuongeza amani na usalama, na pia wanajeshi watapata heshima na hadhi kwa kutimiza madhumuni ya kulinda wananchi na mali zao.

Nina hakika hili linawezekana

5 comments:

Mija Shija Sayi said...

Natamani mheshimiwa rais angesoma hii. Tumekuwa ni watu wa kujipweteka tu.

kamala Lutatinisibwa Lutabasibwa said...

leo sitanii

Mzee wa Changamoto said...

Tatizo sio kuwepo kwa suluhisho Da Mija. Tatizo si kwamba hawasomi wala kuelezwa liliko suluhisho, tatizo si kwamba hawawezi kupata mahala palipo na suluhisho.
TATIZO NI KWAMBA WANAFANYA YOTE HAYO JUU KISHA WANAFUMBA MACHO
WANAPUUZA
Asante kaka. Narejea machimboni

Mija Shija Sayi said...

Nikiongezea kwa mzee wa Changamoto,...Halafu hakuna kitu kigumu kama kumbadilisha mtu anayefanya makusudi hali akijua litakiwalo kufanywa ni lipi.

o'Wambura Ng'wanambiti! said...

Huwa hatuna kizuri cha kujifunza kwa wenzetu bali tunapuyanga tu kivyetu!